Saturday, May 30, 2009

LEO NI SIKU YA AKINA MAMA HAPA SWEDEN =(MORS DAG)


Hapa Sweden leo ni siku ya akina mama duniani. Nasi leo tumeamua kumpongeza mametu mpendwa ktk blog yake ni sisi Camilla na Erik. Tunampenda sana mametu hasa akiwa na hasira, huwa tunapata kila kitu tutakachotaka.( kwa niaba ya mama)

Ok, basi nami nimepata nafasi ya kusema machache ni kwamba. Najua sehemu nyingine siku hii imeshapita ila hapa Sweden ni leo. nami napenda kuwapa pongezi akina mama wote duniani bila kumsaau mamangu. NAWAPENDA AKINA MAMA WOTE DUNIANI.NA TUTAFIKA TU.

UJUMBE WA LEO

Kila siku nimekuwa nikiwaza ipi ni afadhali:
Mnajua ya kwamba afadhali mtu akupige makofi/viboko. Kuliko kumpiga mtu kwa maneno/ kumdharau. Kwa saabu kuna watu ambao hawawezi au hawataki kumpiga mtu ila maneno yake asemayo yanaonekana ni kama kipigo. Au wenzangu mnaonaje?

Friday, May 29, 2009

JE MWENZANGU NI LINI MARA YA MWISHO UMEKULA MUWA?


Hapo kazi na mtu nipo katika shamba langu la miwa, nakata miwa kuwahi sokoni.

Thursday, May 28, 2009

BAADHI YA MANENO YA KISWAHILI NA MAANA YAKE SEHEMU YA KWANZA

Leo nimeona nijikumbushe kidogo maneno ya kiswahili kisije kikaniacha. Kama si sahihi naomba msaada:-

Muungwana = Mtu mwenye adabu na desturi njema, mtu anayekaa na binadamu wenzie kwa uzuri, mtu mwenye utu. Pia unaweza kusema mtu asiye mtumwa au jina la heshima analoitwa mtu.

Mvumilivu = Mtu anayestahamili taabu au mambo mazito (mstahamilivu).

Ngangari = Mtu mwenye msimamo.

Fadhila = Wema, ukarimu, hisani, huruma.

Wema = Ni hali ya matendo mazuri.

Ukarimu= Utoaji vitu au mali kwa kukaribisha watu au kuwasaidia wanaohitaji msaada bila ya malipo. Ni kinyume cha ubahili.

Hisani = Moyo wa kutaka kutenda mazuri kwa ajili ya mwingine.

Huruma = Moyo wa wema; imani, rehema na upole.

1. Imani ni mambo anayokubali mtu kuwa ni ya kweli na anayopaswa kuheshimu hasa katika dini: itikadi. Na pia ni maoni ya moyo yanayomfanya mtu awe na mkabala fulani juu ya jambo au kitu.

2. Rehema ni neema anazopata binadamu kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Na neema ni hali ya kuweko na uwingi wa nafasi; hali ya kutoweko shida au upungufu wa vitu vya kumuendeshea binadamu maisha; baraka na ustawi. Pia ni jambo jema analopata kiumbe kutokana na uwezo wa Mwenyezi Mungu; riziki.

3. Upole ni hali ya kutopenda fujo, hali ya mtu mtulivu na mtaratibu.

Thamini = Gharama au ubora wa kitu kutokana na hali na kuhitajika kwake na jamii.

Na mwisho ni, Si bitozi = Asiyejisikia.

Wednesday, May 27, 2009

MLIMA WETU KILIMANJARO+JIOGRAFIA


Mlima Kilimanjaro ni mrefu kuliko yote Afrika mita 5895. Ni mlima wa asili ya volkeno. Kilele chake kimefunikwa na theluji.

Tuesday, May 26, 2009

WATOTO WENYE ULEMAVU NA MARADHI YA KUDUMU.

Ulemavu wa viungo nao sababu zake zinafanana kabisa na zile za mtindio wa ubongo. Kama nilivyoeleza katika makala yangu moja wiki mbili zilizopita .

Kwa mfano, zipo baadhi ya dawa hasa za kutuliza maumivu ambazo zinapotumiwa na akina mama wajawazito, husababisha kuzaliwa kwa watoto wenye upungufu wa viungo au vilema (Deformed Children).

Ipo sababu nyingine ya kibaiolojia inayotokea wakati wa kutunga mimba. Hata hivyo unapotaka kuzungumzia jambo hili inahitaji ushahidi unaojitosheleza.
Ajali pia ni mojawapo ya sababu zinazopelekea ulemavu wa viungo. Kwa mfano, ajali ya gari, kuanguka na kuumia michezoni, zote hizi husababisha ulemavu wa viungo wa kudumu.

Ulemavu huu unaweza kusababisha hali ya kupooza (Paralysis), kukosa uwezo wa kutembea au hata kupoteza nguvu za kiume. Inawezekana umeshawahi kusikia au kuona mtu aliyeumia mpirani au kuanguka juu ya mti na kupata ulemavu wa kudumu.

Leo ningependa kuzungumzia zaidi tatizo la kupooza ambalo huwapata watu wengi.

Kwanza kuna kupooza kunakoanzia katika sehemu ya kiuno kwenda chini miguuni kwa lugha ya kitalamu kunaitwa paralplegic.

Pili kuna kupooza kunakoanzia shingoni kuja mabegani na kwenda chini miguuni kunakofahamika kitaalamu kama Quadriplegic. Watu wenye matatizo haya huhitaji kiti chenye magudumu ili waweze kutembea. Hata hivyo watoto wenye ulemavu unaoambatana na hali ya kupooza huweza kusaidiwa kwa kutumia njia zifuatazo.

Wazazi wenye watoto wanokabiliwa na tatizo hili wantakiwa wazitengeneze nyumba zao kwa kuzingatia hali halisi ya maradhi ya watoto wao. Kwa mfano wanapaswa kutengeneza njia ambayo itatumika katika kupitisha kiti cha magurudumu badala ya ngazi, vitu ama vifaa vya kuchezea vya watoto wa aina hii sharti vihifadhiwe kwenye kabati ambalo litawekwa kwenye sehemu ya wazi ambayo mtoto anaweza kuifikia na kuchukuwa vitu anvyohitaji bila kuomba msaada.

Pia ianshauriwa kuwaeleza watoto wenzake pale nyumbani au hata wale watoto wa majirani kuhusu ulemavu wa mwenzao, kwamba ni kitu ambacho kinaweza kumtokea mtu yeyote ikiwa ni pamoja na wao, ingawa wamezaliwa wakiwa na viungo kamili.

Hii itawajenga kisaikolojia watoto hao wasimtenge au kumdharau mwenzao ambaye ni mlemavu.

Watoto wa aina hii haitakiwi kuwaonesha kwamba hawawezi kufanya kitu chochote. Hivyo inashauriwa kuwajengea tabia ya kujitegemea kwa kuwaruhusu wafanye yale wanaoweza kuyafanya, kwani kwa kufanya hivyo kutawajengea hali ya kujiamini.

Je watoto wenye maradhi ya kudumu wanasaidiwaje?
Watoto wenye maradhi ya kudumu kama vile pumu, kisukari au kifafa ni miongoni mwa watoto wenye kuhitaji msaada maalum, inashauriwa kuwafahamisha watoto hao juu ya maradhi yanayowa sumbua ili wayafahamu na kuyazoea, pia hata wanafunzi wenzao au watoto wa majirani ni vema pia wakafahamishwa kuhusu maradhi yanayowasumbua wenzao kwani itasaidia kupunguza utani na dhihaka dhidi yao. Kwa upande wa waalimu inashauriwa kuwa watoto wa aina hii upendeleo na uangalizi wa karibu pale inapobidi kulingana na tatizo la mtoto husika.

Ukweli ni kwamba kuzaa mototo mwenye matatizo niliyoyaeleza siyo dhambi na wala hatupaswi kuwatenga watoto au watu wa aina hii, kwani wakipatiwa elimu bora na ya kutosha wanaweza kabisa kujitegemea kwa kufanya kazi za aina mbalimbali na kulipa kodi na kuchangia pato la Taifa. Kama nilivyosema katika mada iliyopita kwamba sio lazima wawe na kazi ya maana ila cha msingi ni kuwa na kitu cha kufanya.

Monday, May 25, 2009

Sunday, May 24, 2009

KWA NINI WATU WANAOANA?

Kama ukimuuliza au ukiwauliza watu wanaooana, kwamba kwa nini wanaoana au ni kwa nini wako kwenye ndoa? Utapata majibu tofauti tofauti kulingana na namna watu hao wanavyotafsiri neno ndoa. Mimi sitajibu swali hilo lakini labda kile ninachokusudia kukiandika hapa huenda kikakusaidia kupata jibu la kwa nini watu wanaoana.

Kuna ukweli kwamba binadamu wamefanya kuoana kama jambo la kimaumbile, na wakilifunganisha na tendo la ndoa. Mtu anajikuta akioa au kuolewa tu. Hana haja ya kujiuliza ni kwa nini anaoa au kuolewa, kwa sababu anaona watu wanoa na kuolewa na akiangalia umri wake anaona kwamba amefikia umri wa kuoa au kuolewa hana haja ya kutaka kujua sababu. Hivi ni nani aliyepanga umri wa kuoa au kuolewa? Na umri wa kuoa au kuolewa umapangwa kwa kuzingatia vigezo gani? Je kupitisha umri huo kuna athari gani?

Ipo sababu nyingine inayotajwa kuwa watu wanoana kwa sababu wamependana, upendo ninaouona hapa ni wa mtu kumtamani mwenzie awe mwanamke au mwanaume, kwani kwetu sisi tunaamini kuwa kutamani ndio kupenda.

Hivi kam watu wanoana kwa sababu ya kupendana kungekuwa na talaka kweli? Naamini kama kungekuwa na talaka basi zingekuwa ni chache sana, na wanaoachana wasingeachana kwa ugomvi na visasi, bali wangeachana kwa upendo na wangeendelea kupendana na kuheshimiana, kwa sababau upendo ni tofauti na kutamani, upendo upo na utaendelea kuwepo na si vinginevyo.

Utakuta wanandoa wanasema “sisi tumeoana kwa sababu tunapendana” lakini baada ya mwaka wanandoa hao hawaelewani na wanakuwa na ugomvi wa mara kwa mara mpaka kufikia mmoja kumuua mwenzie, huu ndio upendo wa aina gani?

Ndoa za namna hii, hazikuwa ni za upendo bali watu kutamaniana au mtu kutamani mwili wa mwenzie, lakini kulikuwa hakuna upendo miongoni mwao.

Wengi wameoana kwa kufuata mnyororo ule ule wa kuoana kwa kufuata dhana iliyowekwa na jamii kuwa ni lazima watu waoana bila kutafuta tafsiri ya kufanya jambo hilo. Na mara waingiapo katika ndoa huona kama wamejitwisha mzigo mzito wasioweza kuubeba. Kuna zile kauli zinazotolewa ambazo wengi huita usia kwa wanandoa kwamba ndoa ni kuvumialiana, lakini watu hawajiulizi ni nini maana ya kuambiwa ndoa ni kuvumiliana, kuvumiliana kwa lipi? Kuna kitu gani katika ndoa kinachohitaji watu kuvumiliana?

Haya maswali inapaswa watu wajiulize kabla hawajaingia katika ndoa maana kuna mambo mengine hayafai kuvumilia, sasa itakuwaje nikishindwa kuvumilia? Na kuvumilia huko ni mpaka wapi?

Kuna watu wengi wanapata shida katika ndoa kwa sababu hawakujua ni kwa nini wanaoa au kuolewa, inawezekana, waliunganishwa na tendo la ndoa zaidi na sio upendo, na hapo ndipo wanpokuja kugundua kuwa walifanya makosa.

Nadhani imefikia wakati sasa ya watu kujiuliza ni kwa nini wanaoa au kuolewa, kwani ni hii itapunguza magomvi na talaka katika ndoa.Inabidi kila mtu awe na sababu yake mwenyewe ya kuamua kufanya hivyo sio kwa kuangalia sababu zilizowekwa na jamii au kusukumwa na matakwa ya jamii bali uwe ni uamuzi wake mwenyewe bila kushurutishwa au kusukumwa na matakwa ya jamii.

Kama hujaoa au kuolewa isikupe shida tulia, na ukitaka kuoa au kuolewa ufanye hivyo ukiwa na sababu yako binafsi.

Saturday, May 23, 2009

KARIBUNI TUJUMUIKE (CHAKULA NI UHAI) + MAISHA


Chakula ni muhimu hapa ni ugali, kisamu, kachumbali na samaki karibuni sana!!!!

Friday, May 22, 2009

HIVI KWELI FURAHA NI KITU ADIMU?

Mara nyingi napatwa na hasira sana na pia uchungu.Yaani ninaposikia watu wanasema, fulani yule anaishi maisha mazuri mwenzetu. Yaani watu wanafikiri kuwa na gari nzuri, nyumba nzuri nguo nzuri basi akili zao zinawatuma ya kuwa huyu mtu/mwenzetu sio mwenzetu ana furaha na pia raha sana. Kwa kweli sio hivi:- unaweza ukawa na vitu vyote hivyo na ikawezekana maisha yako hayana furaha. Kwani FURAHA sio vitu.

1. Furaha ni kuwa na marafiki/rafiki wenye/mwenye furaha.

2. kuwa na furaha unaweza ukawa na furaha hata kama huna mali yaani vitu vizuri. Nina maana FURAHA NI MUHIMU KULIKO PESA.

3. Pia furaha ni kuamka kila asubuhi na kujua kuwa ni mzima wa afya pia kuwa na familia ambayo inakujali na kukupenda wewe kama wewe.

Mtu /watu mwenye/wenye furaha huishi maisha marefu.

Thursday, May 21, 2009

AMA KWELI DUNIANI TUMEZALIWA WAWILIWAWILI

Je? mnawafahamu hawa watu ni akina nani? je? unadhani ni pacha? au dada na kaka?

Wednesday, May 20, 2009

JINSI YA KUCHEZA NA HERUFI

NATAKA KUSEMA KWA YEYOTE YULE:-

U= Ulale

S= Salama

I = Ila

K= Kumbuka

U= Ukiamka

M= Mshukuru Mungu

W= Wako

E= Elewa kuwa

M= Mungu wako

A= Anakupenda

KATIKA MAISHA NI VIZURI KUWAFARIJI MWENYE MATATIZO

Huu ni ushauri wangu mimi kwa wewe uliye na rafiki aliye na matatizo:-

1) Kama rafiki yako ana matatizo usiogope kumwuuliza hali yake kwa ujumla hata kama hali yake inaonekana si nzuri. Kama una matatizo halafu watu/marafiki wanakuuliza U HALI GANI utajisikia amani yaani kuna watu ambao wanakujali haupo peke yako.

Wakati mwingine kunatokea mambo, ambayo si kweli na watu wanafikiri kuwa tayari yule mwenye matatizo amepata msaada. Yaani mtu wa kuongea naye. Wakati kumbe wewe upo peke yako kwa hiyo kuuliza ni muhimu sana.

2) Piga simu au nenda ili kujua mpatwa matatizo ana hali gani. Pia pika chakula, nenda kwake na mle pamoja. Wakati matatizo yanapotokea, inakuwa ngumu kuelezea vitu ulivyozoea kufanya kila siku. Kama una watoto inakuwa ngumu zaidi kuwatunza wakati upo kwenye matatizo/majonzi. Kwa hiyo ni vizuri kusaidiana.

3) Onyesha upendo wako, bila kuonekana ni usumbufu kwa mpatwa matatizo, uwe nusu nusu. Usizidishe au usipunguze. HAPO NDIPO UTAWEZA. Kama nilivyosema hapa juu huu ni ushauri wangu mimi.!!!!

Tuesday, May 19, 2009

LEO TUANGALIE MAMBO YA MAPISHI PIA KWANI BILA KULA HATUWEZI KUISHI

Chakula chenyewe si kingine ni Maandazi

5 VIKOMBE VYA UNGA WA NGANO.

* 1 ¼ VIKOMBE VYA TUI LA NAZI ZITO VUGU VUGU.

*3/4 KIKOMBE CHA SUKARI.

* 3 VIJIKO VYA KULIA VYA SAMLI ILIYOYAYUSHWA AU MAFUTA

*1 KIJIKO CHA SOUP HAMIRA.

*1/2 KIJIKO CHA CHAI CHA HILIKI YA UNGA.

*MAFUTA YA KUKAANGA.

NAMNA YA KUTAYARISHA NA KUPIKA:

1.Ndani ya kibakuli kidogo, mimina hamira na na vijiko viwili vya kulia vya tui. Weka kando mpaka hamira ianze kufura, kama dakika 5-10.

2.Pasha samli moto

3.Ndani ya bakuli kubwa au sinia, changanya unga, sukari, iliki na samli ikiwa bado moto moto.

4.Mimina hamira ndani ya mchanganyiko wa unga. Changanya na ukande huku ukitumia lile tui la nazi. Tui likipungua unaweza ukaongeza maziwa. Kanda unga mpaka uwe laini.

5.Kata madonge *12 au 15 uyaweke kwenye baraza iliyonyunyiziwa unga na uyafunike ili yapate kufura na yasikauke.

*Ukipenda maandazi manene fanya madonge 12. Ukipenda mepesi fanya madonge 15


Kabla ya kuumuka (kufura)

Baada ya kuumuka (kufura)

6.Madonge yakifura, sukuma kama chapati kisha ukate mara nne kama kwenye picha. Endelea kufanya hivyo na madonge yote. Yawache maandazi yafure tena baada ya kukata kama dakika 15 hivi.


7. Pasha mafuta moto kwenye karai. Maandazi yako tayari kukaangwa sasa.

8.Kaanga maandazi kwenye mafuta ya moto. Upande mmoja ukifura na kuwa rangi nzuri geuza upande wa pili. Endelea nama hii mpaka maandazi yote yawe tayari.



TIPS ZA KUHIFADHI MAANDAZI

1.Unaweza kuweka unga wa maandazi uliyokwisha kuyakata ndani ya freezer yakisha umukua ikiwa unataka kutumia siku nyengine. Tumia waxed paper na unga wa kutosha kuweka katikati ya maandazi ili yasishikane unapoya freeze kwanza katika freezer. Yakishika barafu, toa na yafunike kwa wax paper kiasi kama matano pamoja na uyatie katika freezer bags. Ukitaka kukaanga maandazi siku nyengine, toa maandazi mapema kidogo yatoke barafu kidogo tu. Pasha mafuta moto kwenye karai na kanga maandazi.

2.Vile vile unaweza kuyapika kabisa na kuweka katika freezer bags, ukitaka kutumia ni kuyatoa tu na kupasha moto katika Microwave.

Monday, May 18, 2009

MISEMO /ORDSPRÅK

Ngoja leo tuangalia misemo yetu nimeona niandike lugha zote mbili.


Kiswahili: Kwa kila dakika uwepo na hasira, unapoteza sekunde sitini za furaha yako.
Svenska/kiswidi: För varje minut som du är arg, förlorar du sextio sekunde av glädje.

Kiswahili: Ni afadhali kupoteza maneno kwa uzuri kuliko kukusanya.
Svenska/Kiswidi: Det är bättre att slösa med vänliga ord än att samla på dem.

Kiswahi: Kila kitu kinahitaji uamuzi.
Svenska/kiswidi: Mycket handlar om beslutsamhet.

Kiswahili: Watu wengi wanataka kuwabadili wengine kuliko kujibadili wenyewe
Svenska/Kiswidi: Många människor vill hellre förbättra anda än sig själva

Kiswahili: Si muhimu wapi unatoka isipokuwa wapi unakwenda.
Svenska/Kiswidi:Det viktigaste är inte vårifran man kommer, utan var man går.

Kiswahili: Tupa likusumbuala, pokea lichangamshalo
Svenska/Kiswidi: Släng ut det som stör, led in det som stimulerar.

Kiswahili: Anayeacha kuwa bora anaacha kuwa mwema.
Svenska/Kiswidi: Den som slutar att bli bättre slutar att vara bra

Kiswahili: Kama hali inakuwa mbaya rudi nyuma na uangalie vizuri
Svenska/Kiswidi: När allt verkar hopplöst ta då ett steg tillbaka och lift blicken.

Sunday, May 17, 2009

JUMAPILI NJEMA KWA WOTE

JE? TUNAZINGATIA HAYA KATIKA MAISHA YETU YA NDOA

PICHA NA MAKALA KUTOKA KWA http://mbilinyi.blogspot.com/


Kumpata mwenza au mke au mume ambaye utaishi naye maisha yako yaliyobaki hapa duniani ni jambo la msingi sana katika maisha ya binadamu.
Na kwa kupenda wenyewe hupelekana hadi kwa viongozi wa dini na kutangaza hadharani kwamba mimi na mwenzangu tunataka kuwa mke na mume na ulimwengu ujue.
Huwa tunakuwa tumejawa na mioyo yenye furaha na kutaka siku ifike upesi ili nianza kuishi na mwenzangu haraka iwezekanavyo.

Mungu bariki mioyo ya maharusi wapya maana hawajui kazi halisi wwanayoenda kuianza kazi halisi maisha ya kweli na kuachana na maisha ya uchumba ambayo mengi ni tambarare kama nyikani.
Baada ya honeymoon tu wengine siku ya pili tu, wengine mwezi wa kwanza tu na wengine mwaka wa kwanza tu wa ndoa huanza kujiuliza hili swali;
Lakini hakuna aliyeniambia itakuwa kama hivi?

Alikuwa anaacha mialiko ya watu kwa ajili yako lakini baada ya kukuoa si hivyo tena, unadhani kwa kuwa alikuwa ana cancel futa mialiko ya kwenda kufanya mambo yake kwa ajili yako kabla hamjaona na mkioana itakuwa sawa?
You are wrong! Unakosea

Ili usipoteze matarajio ya mahusiano yako ya ndoa jaribu kuzingatia mambo yafuatayo (kama unategemea kuoa au kuolewa please print na kafiche haya unaenda kuyasoma na baada ya kuanza ndoa soma tena na pia ukiyaweka moyoni na ukizingatia utakuwa candidate mzuri sana)

Hakuna binadamu anaweza kutimiza mahitaji yako yote:
Mtu ambaye anaweza kutimiza mahitaji yako yote ni BWANA, na ilimpasa kufa ili aweze kukutimizia yote.
Usitegemee ndoa au uliyeoana naye atakutimizia mahitaji yako yote au ahadi zake zote alizoahidi kabla hamjaoana.

Kiwango cha mapenzi hakiwezi kuwa juu kama ilivyo mwanzo wa ndoa.
Jinsi anavyokwambia "nakupenda” huweza kupungua hadi ukashangaa kadri ziku zinaenda ingawa neno ”nakupenda” huleta raha sana kwa mwanamke akisikia kutoka kwa mumewe hata hivyo siku zinavyoenda mwanaume hujisahau na kuanza kula jiwe kusema “nakupenda”
je, utadai?
Pia wanawake nao (wachache sana) akishazaa huanza kujisahau na kujiona mama na si mrembo bado. Huku ni kukosa ustaarabu na kinyume cha maadali.
shame on you! Muona aibu!

Mwanaume anaweza kuwa anakupenda mno lakini bado hatajua unahitaji kitu gani.
Wanawake wengi huja na sentensi ‘ Kama ananipenda angefanya kile napenda afanye” kumbuka usiposema na kumwambia ujue hawezi kujua unataka kitu gani au nini kinakusumbua.
Kama huulizi basi jibu litakua HAPANA
Men read newspapers not minds! Wanaume wanasoma magazeti sio mawazo

Si mara zote uliyeoana naye atapenda kuimarisha mahusiano.
Katika mazingira ya kawaida wanawake hupenda hata kuimarisha kitu kizuri (mfano ndoa ambayo hata haina mgogoro) hata hivyo wanaume wana msemo wao
“ kama haijakatika , isitengenezwe”
Hivyo tumia hekima na kuomba Mungu ili Mungu awape moyo wa umoja na juhudi ya kuishi kwa amani.

Ndoa haiwezi kukufanya uwe umekamilika.
Si mara zote ukiongeza nusu na nusu unapata kitu kizima.
Wengi ambao ni “hawajaoa” hudhani wakioa au kuolewa watakamilika na kujiona kamili na kuwa na furaha ya kweli.
Na wengine hufika mbali zaidi kwa kujinyima vacation, kununua vitu vizuri wakisubiri kufanya hivyo wakioa au kuolewa.
Unapoteza muda wako anza kukamilika kwanza kabla ya kuolewa au kuoa na ingia ukiwa si tegemezi kwamba mwenzako atakukamilisha hadi kukupa furaha.
Ndoa ni kuunganisha uwezo na ku-balance udhaifu siyo kukaa tu kutegemea mwenzako akukamilishie furaha yako.

Usitegemee kufanya kila kitu pamoja
Kufanya kazi pamoja, kupanga mipango pamoja, kuweka malengo pamoja ni suala zuri sana hata hivyo kila mmoja huhitaji kupumzika/pumua.
Usitegemee kila kile unapenda basi na mwenzio atakuwa excited nacho si kweli hivyo kuna wakati utahitaji kuwa mwenye na yeye kuwa mwenyewe.
Nakwambia mapema ili siku ikifika usiseme hakuna aliyeniambia, mimi nimekwambia!

Mtu ambaye anaweza kumbadilisha ni yeye mwenyewe si wewe.
Kama unategemea ukioa au kuolewa utambadilisha mpenzi wako basi utakuwa very much disappointed. Umesikitishwa sana
Kama kuna vitu vinasumbua kwa mpenzi wako kabla humjaona viangalia vizuri, kutegemea kwamba utamsaidia kubadilika baada ya honeymoon ni kujidanganya kulikokithiri.
Ndoa si mahali pa kulaumiana, kukefyakefya (nagging), hasira na kukosoana.
Kama mpenzi wako hajui UCHAFU ni kitu gani hakikisha anafahamu kabla hamjaoana, na kama unategemea utambadilisha aache ulevi, kuvuta sigara, kuwa mwongo nk shauri yako!

Maswali ya kujadili
Wewe ambaye upo kwenye ndoa sasa je, unaona maratajio yako yote ya ndoa yalitimia?
Je, una matarajio yoyote ambayo unahisi yalikusumbua zaidi?
Je, una ushauri gani kwa wanandoa wapya?

Friday, May 15, 2009

WATOTO NA MATATIZO YA MTINDIO WA UBONGO

Ngoja tuendelee na mada hii lakini samahanini imekuwa kinyume.

Wapo watoto wengi wanaozaliwa wakiwa na matatizo mbali mbali, lakini mojawapo nitatizo la mtindio ya ubongo ambalo leo nimeona nilizungumzia kwa undani zaidi.
Matatizo ya mtindio wa ubongo yanatokana au kusababishwa na kizalia (Genetic), dawa alizotumia mama wakati wa ujauzito, matumizi ya madawa ya kulevya, pombe, hali ya hewa, au hata ajali. Mojawapo ya sababu hizo nilizozitaja zinaweza kusababisha kuzaliwa kwa mtoto mwenye mtindio wa ubongo au mtu kupata mtindio wa ubongo.

Nikianza na tatizo la pombe, ni kwamba pombe ina athari kubwa na mbaya kwa akina mama wajawazito. Lipo tatizo linalofahamika kitaalamu kama Fetal Alcoholic Syndrome (FAS) ambalo huwapata watoto ambao wazazi wao walikuwa wanatumia kiwango kikubwa cha pombe wakati wa ujauzito.

Watoto wanozaliwa na tatizo hili wanakuwa na nyuso ambazo sio za kawaida (FacialDeformities), kwa mfano watoto hawa wanweza kuwa na pua bapa na macho yaliyoingia ndani au kuwa na mtindio wa ubongo (Mental Retardations), matatizo ya kusikia na kutokuwa na uwezo wa kusoma.

Kwa hiyo unywaji wa pombe hata kwa kiwango kidogo katika kipindi cha mwezi mmoja hadi mitatu ya mwanzo kwa mama mjamzito huchangia kwa kiasi kikubwa kuzaliwa kwa watoto wenye matatizo haya.

Watot wote wenye matatizo haya ya mtindio wa ubongo wanaweza pia kujifunza kusoma iwapo watapewa msaada maalum na kuandaliwa mazingira mazuri yatakayowashawishi kujifunza kusoma. Malezi kwa watoto wenye matatizo haya, yanatakiwa yawe tofauti na yale ya watoto wa kawaida.

Watoto hawa wanahitaji kuoneshwa upendo, kusikilizwa na mengineyo ya aina hiyo. Hata hivyo swali la msingi tunalopaswa kujiuliza ni kwamba, tutawatambuaje watoto wenye tatizo hili la mtindio wa ubongo wakingali wadogo?

Ukweli ni kwamba ni vigumu sana kwa wazazi kuwatambua watoto wao wenye tatizo hili, kabla watoto hao hawajatimiza umri wa miaka mitatu au minne. Kwa kawaida inashauriwa kwamba mtoto yeyote ambaye anfanya mambo yake pole pole ukilinganisha na watoto wengine wa umri wake, inapaswa kupelekwa haraka hospitalini kwa daktari bingwa wa watoto ili afanyiwe uchunguzi wa kina.

Hata hivyo dalili zifuatazo zinaashiria kuwa mtoto ana tatizo hili Kwanza haoneshi dalili yoyote ya kulia au anaweza kulia kidogo sana. Pili huchelewa sana kutembea na hata kuongea. Tatu haoneshi kuvutiwa nna mazingira yanayomzunguka, kwa maana kwamba hata kama kuna vitu vya kuchezea hawezi kujishughulisha navyo. Nne ni vigumu sana kufundishika na hata kujifunza kusoma huwa ni kazi ngumu ukilinganisha na watoto wa rika lake.

Tano hawezi kula mwenyewe, kuvaa mwenyewe au kujifunza kutumia choo. Hata hivyo zipo dalili nyingi zinazoweza kujitokeza na mara nyingi zinatambuliwa na madaktari maalum wa watoto.

Jinsi wazazi wanavyoweza kuwasaidia watoto wenye tatizo hili:

Watoto wenye mtindio wa ubongo wanafundishika, iwapo tu watafundishwa kwa makini, utulivu na uvumilivu mkubwa, yaani mtu anayemfundisha mtoto wa aina hii hatakiwi kamwe kuwa na hasira, na pia inashauriwa sana kuwapongeza wanapofanya vizuri japo kidogo.

Mwalimu anatakiwa awe mpole na ufundishaji wake usiwe wa haraka haraka, aoneshe mapenzi kwa mtoto, hapaswi kumkemea hata kama anakaosea .

Watoto wa aina hii inashauriwa wapewe nafasi ya kujenga urafiki na watoto wenzao warika lao. Huko nyuma watoto wenye matatizo ya akili walikuwa wantengwa na watoto wenzao katika madarasa, kwa kuwekwa kwenye madarasa maalum.

Lakini siku hizi inashauriwa wachnganywe na wanfunzi wenzao wasio na matatizo ya akili, japo hata kwa nusu siku. Utaratibu huu hujulikana kitaalamu, kama mainstreaming.Itaendelea.....

NGOJA LEO TUTEMBELEE KIJIJI CHA LIULI


Hap ni hospital ya Liuli

Na hapa ni kanisa la Liuli

Thursday, May 14, 2009

WATU WENYE MTINDIO WA UBONGO NAO NI WATU KAMA SISI

Ni watu ambao akili zao zinachelewa kukua. Mtu mzima, mwenye miaka 60 lakini utamwona akili yake ni kama mtoto wa miaka 3. Kwa kweli ni jambo la kusikitisha sana:- Nasema hivi nikiwa na maana nilikuwa nyumbani TZ. Niliwahi kuona watu wengi wenye watoto wenye mtindio wa ubongo walikuwa wakiwaficha ndani ya nyumba kwa kuona aibu.

Baadaya ya kuishi hapa kwa muda huu nilioishi, nimefanya utafiti na kugundua ya kwamba sisi waAfrika/waTanzania. Kila kitu tufanyacho tupo nyuma yaani tunafanya baada ya wenzetu/Ughaibuni kupiga hatua mbele. Nasi tunafuata nyuma. Ni hivi katika utafiti wangu wao/Ughaibuni pia hapo zamani walikuwa wakipata mtoto mwenye mtindio wa ubongo waliona aibu na hawakumtaka yule mtoto. Walimpeleke kwenye nyumba maalumu. nyumba ya watoto "YATIMA". Ilikuwa ni kinyume na Afrika/TZ wao waliwatunza wenyewe ila hawakutaka waonekane.

Lakini sasa hapa niishipo wenye mtindio wa ubongo wote wanaruhusiwa kufanya chochote kile kutegemea na ulemavu gani anao. Wanaruhusiwa kwenda shule, yaani shule maalumu, wanafanya kazi kulingana na uwezo wao, wanaishi kwenye ghorofani "peke yao" huku wakisaidiwa na wafanyakazi yale mahitaji muhimu. Wamekuwa ni watu wa "kawaida" katika jumuia.

Tanzania pia wamefikia hatua kubwa kidogo ukilinganisha na miaka ya 1980. Kuanzia miaka ya 1990 kulikuwa/kumekuwa na shule ya wenye mtindio wa ubongo. Ila sasa tatizo ni kwamba wakishamaliza pale wanawaacha tu. Hakuna anayewajali watu hawa. Kwa mtazamo wangu naona wao wanaumuhimu wa mahitaji kama sisi wengine. Kwa sababu hawa hawahitaji kazi ya maana sana. Kinachotakiwa ni vijikazi vidogovidogo. Yaani kuwepo na sehemu (nyumba/jengo) ili wawe wanaenda kufanya kazi hata masaa mawili kuliko kuwaacha tu. TUSISAHAU YA KUWA BINADAMU WOTE NI SAWA!!!!

Wednesday, May 13, 2009

HIVI HAPA WAPI? NISAIDIENI BASI


Au Ruhuwiko nini? Mmh! kama, ngoja wasomaji wanisaidie

Tuesday, May 12, 2009

UBAGUZI WA RANGI TANZANIA/AFRIKA

Haya ni maoni ya MAKULILO,Jr kwenye mada ya UBAGUZI WA RANGI TANZANIA/AFRIKA nimeona niyaweke hapa wote ili tujadiliane.

MAUAJI YA ZERUZERU (ALBINO) TANZANIA NAYO NI UBAGUZI WA RANGI

Nimekaa na kufanya tafakari ya kina kuhusiana na mauaji ya ndugu zetu Albino yanayoendelea kuisakama Tanzania. Dhana mbili zinajitokeza katika tafakari hiyo. Moja ni dhana nzima ya ubaguzi wa rangi na pili ni tathimini yangu kuhusu mikakati ya serikali ya Tanzania kuwahakikishia usalama ndugu zetu Albino.

Ukiangalia ubaguzi wa rangi uliokuwepo Afrika Kusini enzi za Makaburu, watu walipangwa katika makundi kutokana na rangi zao; weupe ( Wazungu ), watu wa rangirangi (coloured ) na weusi ( Waafrika ). Huduma zote, ikiwa ni pamoja na elimu, zilitolewa kwa kuzingatia rangi ya mtu.

Kulikuwa na kumbi za starehe kwa ajili ya watu weupe, ambapo mtu mweusi hakuruhusiwa kuingia. Kuna sehemu zingine ambazo mwafrika hakuruhusiwa hata kukanyaga kabisa. Akikamatwa, alipewa kipigo kikali na hata kutupwa lupango ( jela).

Ubaguzi wa rangi, hususani dhidi ya Mwafrika, ulikuwepo hata katika nchi za Magharibi. Nakumbuka nimeona picha zilizoandika “only for blacks and dogs here.” Hii ilikuwa hatari sana, kwani mtu mweusi alinyimwa haki zake kutokana na rangi ya ngozi yake .

Sasa tujiulize.Hivi Albinno ni mtu wa namna gani? Anaweza tambuliwaje kwa muonekano wake? Sintopenda kuingia ndani zaidi kuchimba sababu za kibaiolojia zinazo mfanya mtu azaliwe Albino. Hata hivyo mtu haitaji microscope ( darubini) wala elimu ya Chuo kikuu kumtambua Albino.

Nionavyo mimi, naamini bila pingamizi lolote kuwa mauaji ya Albino yanayoendelea kuitikisa Tanzania “Kisiwa cha Amani” ni mwendelezo wa dhambi ya ubaguzi wa rangi, lakini huu ni ubaguzi mkali zaidi katika historia ya mwanadamu kushinda hata dhambi ya biashara ya utumwa.

Nasema nimkali zaidi kwani unalenga kuondoa maisha ya mwanadamu kwa ukatili wa kunyofoa viungo, tofauti na ule wa kumzuia mweusi kutembelea mitaa fulani au katika upandaji wa mabasi n.k !

Ni kwa kuangalia rangi ya ngozi yake, unaweza kumtambua Albino. Kwa bahati mbaya, Albino anayezaliwa Afrika, ni tofauti na yule wa nchi za Ulaya na Marekani, kwani Albino wa nchi hizo, hatofautiani sana na mtu wa kawaida. Rangi yake inarandana na ya mzungu . Si ajabu kama naye angefanana na mwafrika, angebaguliwa na kuuawa.

Kinachonishangaza mimi, ni kwanini Tanzania au Watanzania kwa ujumla hatusemi ukweli kuwa mauaji ya Albino yanayoendelea, ni ubaguzi wa rangi ili tuweze kupambana nao ipasavyo na Jumuiya ya Kimataifa iweze kutoa msaada sawawa na ambavyo jumuiya ya Kimataifa, hususani Tanzania, ilivyojitoa muhanga kung’oa mzizi wa ubaguzi wa rangi Afrika Kusini?

Kwa mtazamo wangu, Watanzania tumeaminishwa kuwa Tanzania ni kisiwa cha Amani na hivyo sisi ni bora zaidi kuliko Taifa lolote kiutamaduni na kimaadili. Hii si kweli na huu ni mtazamo potofu ambao tusipokuwa makini, utatufikisha pabaya.

Kwa uzoefu wangu, kitendo cha ubaguzi kikifanywa na Taifa jingine mfano Burundi, Kongo, Afrika Kusini, Ujerumani, M arekani ama Israeli, tunawanyooshea kidole kuwa wamepotoka huku tukitamka wazi kuwa nchi hizo zinafanya ubagauzi wa rangi. Je, kwa nini kitendo hicho kikitendeka Tanzania kama cha mauaji ya Albino, tunapata kigugumizi kutamka wazi kwamba ni kitendo cha ubaguzi wa rangi na tunaanza kutafuta majina mengine kama vile “unyanyasaji wa Albino” na k.n yasiyotoa picha halisi ya mambo yanayoendelea?

Kwani ubaguzi wa rangi lazima kitendo kifanywe na mtu mweupe ( mzungu ) dhidi ya mweusi ( mwafrika ) ili kistahili kuitwa ubaguzi wa rangi? Vipi kama kitendo hichohicho kitafanywa na mtu mweusi dhidi ya mtu mweupe ( mzungu / albino ), hakiwezi kuitwa kitendo cha ubaguzi wa rangi?

Au kama mtu mweusi atafanya kitendo cha kumbagua mweusi mwenzake kutokana na rangi yake kama vile mweusi sana , mweusi tiii! mweusi wa kati, nacho hakiwezi kuitwa ubaguzi wa rangi? Na vipi kama mtu mweupe ( mzungu ) akimbagua na kumnyanyasa mweupe mwingine kama vile Mchina , Mwarabu n.k, kitendo hicho kitaitwaje?

Kwa uzoefu wangu, hasa baada ya kuangalia matukio ya hivi karibuni ambapo Waafrika Kusini waliamua kuwavamia na kuwaua wahamiaji kutoka nchi nyingine za Afrika, Tanzania ilikuwa mstasri wa mbele kukemea vitendo hivyo. Tanzania ilitoa tamko kali na kwa uwazi kabisa ikisema, “ Dhambi ya ubaguzi bado inaitafuna Afrika kusini.”

Nikaanza kuangalia mambo mengine ninayoyashuhudia kila kukicha huku Marekani. Mtu akifanyiwa kitendo fulani, kwa mfano, ikiwa ni mweupe kakifanya, hukimbilia kusema ni ubaguzi wa rangi.

Sasa mimi najiuliza. Je endapo Mtanzania mweusi mmoja ataenda nchi yoyote ya Magharibi kama vile kusoma au kufanya kazi halafu akauliwa na kunyofolewa viungo kama wanavyofanyiwa Albino, Tanzania itasemaje? Haina ubishi , kila mtu atasema “amebaguliwa na kuuwawa kutokana na rangi yake.”

Swali langu la msingi ni hili: Kitendo cha Albino kunyofolewa viungo vyake kinyama na hatimaye kuuawa na mtu mwenye rangi nyeusi kisa rangi yake ni tofauti na cha mtanzania mweusi aliyebaguliwa na kuuawa ugenini hususani katika nchi za magharibi? Kwa nini mauwaji ya Albino yasitajwe kama ubaguzi wa rangi? Maana Albino naye hutambuliwa kwa rangi yake!

Kama tumefikia hatua ya kuuana kutokana na rangi zetu; moja nyeusi, nyingine ya rangirangi ( coloured ) na wote ni binadamu tena watanzania, tuanaelekea wapi ndungu zangu?

Serikali ya Tanzaia inaendelea kuchukua hatua mbalimbali kupambana na janga hili la mauaji ya albino. Uamuzi wa kugawa simu kwa albino wote, pengine waweza kusaidia kwa kuwawezesha kupiga simu polisi wanapovamiwa.

Lakini Serikali inawasaidiaje albino waishio kijijini ambako hakuna umeme? Simu hiyo inachajiwa kwa teknolojia gani? Je simu hizo hizitakuwa kivutio kingine na hivyo kuwafanya wavamiwe zaidi?


Kama imefikia hatua albino hawezi kutembea peke yake au kutembea baadhi ya masaa hususani jioni, kama imefikia hatua Mbunge maalum ambaye ni albino lazima apewe ulinzi maalum ili asinyofolewe viungo vyake, falsafa ya Tanzania kama kisiwa cha amani iko wapi?

Ndugu zetu wa Marekani wanaelekea kuishinda dhambi ya ubaguzi wa rangi, kwani hatimaye wamefikia hatua ya kumchagua mtu mweusi kuwa Rais wao kwa kuangalia uwezo wake, hoja zake na si tena kigezo cha rangi kama Dr. Martin Luther King Jr aliposisitiza katika ndoto yake ( I HAVE A DREAM). Mwaka 2010 kama mgombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania atakuwa albino, tutakuwa tayari kumpigia kura endapo atakuwa na sifa za kutuongoza? Tafakari, Chukua hatua.

Nawasilisha hoja!

MAKULILO, Jr.
Fulbright Visiting Scholar
Blog: www.makulilo.blogspot.com
E-Mail: msauzi101@yahoo.com
West Virginia, US

TUDUMISHE UTAMADUNI WETU WA ASILI


Hapa ni barabara ya Morogoro-Iringa niendapo Songea lazima nisimame na kununua kitu.


Watu tunatoka mbali, watoto wanacheza kuwa wao ni akina mama. Nimekumbuka mbali sana!!

Monday, May 11, 2009

UTARATIBU WA KUTATANISHA WA MANENO(mashairi hafifu)

Je? kuna anayeweza kusema sentensi hii bila kupumzika au kupemua mpaka mwisho. Jaribu ni moja ya mazoezi ya mdomo, huwa nasema hivyo kila asubuhi niamkapo. KARIBUNI!!

Katibu kata wa kata ya mkata amekataa kata kata kukata miti katika kata ya mkata.

NIMERUDI TENA SONGEA HAPA NI CHUO CHA UALIMU SONGEA (KIPO MATOGORO)

Saturday, May 9, 2009

WANAUME WASIOTOSHEKA(WAKWARE) WANAUME WOTE WANA NYUMBA NDOGO?

Sijui nianze vipi hili jambo limekuwa likinitatanisha sana afadhali niliweka wazi ili nisaidiwa nisije nikapasuka kichwa kwa kuwaza. Ni hivi: babu, baba, kaka au nisema wanaume kwa ujumla kwa nini wanapenda kujitoa katika mambo mengi. Nisemapo hivi nina maana mara nyingi utasikia, yule mwanadada/mwanamke ni mhuni/malaya sana Je huu uhuni/umalaya anafanya na nani?. Anajifanyia peke yake?. HAPANA kwa sababu kuna wanaume wasiotosheka, wenye tamaa wanawaacha wake zao nyumbani na kwenda pembeni. Na baadaye wanageuka na kusema wanawake wahuni. Mnajua mimi bado sijaelewa kabisa nani ni mhuni hapa. Kwasababu sijawahi kusikia hata siku moja , ikisemwa mwanaume yule mhuni.

Najua wanaume wengi watasema/jitetea ya kuwa hawatosheki na wake zao kwa sababu ya migogoro nyumbani hiyo ndiyo sababu wanatoka nje. Lakini kumbuka hii ni kisingizio tu cha kutoka nje( kuwa na nyumba pembeni)

Inasemekana wanaume hawawezi kuvumilia angalia wanaume waliooa wanaozungukwa na makarani wengi au wafanyakazi wengine ambao ushawishi na mvuto wao wa kimwili unaonekana kila saa katika wakati wa kufanya kazi basi hapo kishawishi tayari.

Nimeona niambatanishe na MADA hii hapo chini kwani inalenga jambo hilo hilo kutoka kwa http://kaluse.blogspot.com/

WANAUME WOTE WANA NYUMBA NDOGO?

Kuna idadi kubwa sana ya wanawake kuliko mimi na wewe tunavyoweza kufikiri, wanaoamini kwamba wanaume wote wana nyumba ndogo. Je wewe mwanamke ndivyo unavyoamini? Je wewe mwanaume umeshawahi kuambiwa hivyo na mkeo au mpenzi wako? Kama bado basi wewe una bahati.

Kwa nini wanawake hawa wanaamini hivyo? Kuna sababu kubwa moja tu ambayo ndiyo yenye kufanya imani hii kushika mizizi, nayo ni malezi. Wanawake kama ilivyo wanaume wamelelewa kwa kuamini kwamba wao ni dhaifu na wanaume ni imara. Wamelelewa kwa kufundishwa kwamba wao hawana haki zote ndani ya nyumba kama ilivyo kwa wanaume.

Katika kuamini huku wanawake wamejikuta wakiwa ni aina ya watumishi ndani ya ndoa na wamejikuta wakiwa ni watu wa jikoni ndani ya ndoa na waamejikuta wakiwa watu wa kupewa amri na kuzipokea ndani ya ndoa. Katika mkabala huo wanawake wamejikuta wakiwa hawana kauli wala sauti hata katika maswala ya kimaumbile.Kwa mfano ni mwanamume ndiye anayetakiwa kusema ‘leo sijisikii’ na siyo mwanamke na ni mwanaume anayetakiwa kusema ‘leo nahitaji’ na siyo mwanamke.

Mwanamke anapokua na mahusiano na mwanaume mwingine nje, anapewa haraka jina la ‘Malaya sana’ wakati mwanaume anaweza kupewa jina la sifa “mkali” au “mtu wa watoto” hata kama ana mahusiano na wanawake kumi. Hii sio nasibu ya mambo bali matokeo ya malezi yetu.

Kwa kupewa nafasi kama hii mwanaume amekua huru kushiriki tendo la ndoa kwa kadri atakavyo kwenye familia zetu. Nyumbani hua tunaona jinsi watoto wakiume wanapokua na marafiki wa kike lisivyo jambo la ajabu , bali tu pale watoto wa kike wanapo jaribu kuwa na marafiki wa kiume hata wale makaka ambao wao huwachezea madada wa wengine huko nje huwa wakali sana kwa madada zao.

Kwa mkabala kama huo, kwenye jamii yetu mwanamke kua mcheshi, mzungumzaji huru na mkaribishaji mzuri kuna maana moja tu kwamba huyu ni malaya, bali kwa mwanaume sifa hizo hubaki hivyohivyo na pengine kuongezewa uzito. Hata kama ndani ya sifa hizo kumejificha ufuska ulio kubuhu, hakuna atakayejali sana.

Kuna ukweli kiasi fulani kwamba, wanaume wengi huwa wana ‘nyumba ndogo’ au zaidi ya rafiki mmoja wa kike. Hali hii imepelekea hata watu kuamini kwamba wanaume wana hamu kubwa na tendo la ndoa kuliko wanawake, jambo ambalo limekanushwa na tafiti nyingi zilizofanywa kuhusiana nalo.

Wanaume kwa sababu za kamalezi na ubabe ulio katika mazoea ya kimapokezi tangu kale, wanaamini kwamba wao ndio wenye uhuru wakuchagua kama waendelee kua na mmoja au hapana. Kwa hiyo,kwa sababu wao ndiyo ambao wamejipa funguo ya maamuzi hufanya uharibifu mwingi.

Kwa kuwa wanaume wanaamini kwamba wanapaswa kuabudiwa na wanawake, linapotokea tatizo dogo tu la kindoa huamua kutoka nje, kwa sababu wanawake kwao ni vyombo vya starehe vinavyoweza kununuliwa mwanamume anapojisikia. Lakini pia hii ni kwa sababu, kutoka nje kwao ni aina ya sifa wakati mwingine.

Kutokana na malezi haya ambayo yanahalalisha mwanaume kuwa “kijogoo” wanaume wengi wamekua na urahisi wakutokua waaminifu . Lakini hata hivyo,hakuna ukweli kwamba wanaume wote wana nyumba ndogo. Nadhani unajua tofauti kati “wote” na “wengi”

Ni vigumu kusema idadi halisi kwa maana asilimia, kwani hakuna utafiti rasmi ambao umefanywa, lakini kwa utafiti usio rasmi imethibitika kwamba kwa hapa Jijini Dar es salaam, kuna uwezekano mkubwa kwamba katika kila wanaume kumi, saba wana ‘nyumba ndogo’ au rafiki wa kike zaidi ya mmoja.

Idadi hii ni kubwa sana na kuna haki kwa watu kuamini kwamba kila mwanamume ana ‘nyumba ndogo’. Lakini bila shaka umefika wakati kwa wanaume kujiuliza kama tabia hiyo ina manufaa yoyote kwao na kama huko sio kuwazalilisha wake au wapenzi wao. Je, wake zao wangekua wanafanya hivyo wao wangejisikia vipi,au wanadhani wanawake hawana hisia kama binadamu?

Friday, May 8, 2009

MWENZENU LEO NIMEAMKA NA KUMKUMBUKA KWELI MAMA YANGU

TUENDELEE KUANGALIE SURA YA KIJIJI CHA LIKUYU FUSI SEHEMU YA NNE= KUNYUMBA

Nimeona afadhali nimalizie kuhusu Likuyu Fusi leo.

Baada ya muda mateka hao walipewa ruhusa ya kuoana na kuzaa watoto. Watoto hao wote walikuwa mali ya Mtepa na waliitwa “Gama”. Wakati wote wa maisha yao walikuwa chini ya nyumba ya Mtepa hata baada ya kufa kwake. Kimila hawa wanaitwa “Gama wa Chikopa”. Mfano mwingine, yupo mzee Zawemba Gama, alipokufa aliacha mke Mzinati mwenye watoto wawili. Baada ya kuondoa tanga bibi Mzinati alipewa ruhusa ya kuolewa na mume mwingine. Akaolewa na Kajanja Komba. Kajanja hakutoa mahari ya kumwoa Mzinati badala yake alitoa mbuzi mmoja dume kwa ndugu wa Zawemba kuwaomba kuwa anataka kuishi na bibi Mzinati. Hivyo Kajanja aliruhusiwa kumchukua Mzinati kwa masharti kuwa watoto wote watakaozaliwa watakuwa mali ya “Gama”. Kajanja hakuwa na haki juu ya watoto, ingwa watoto hawa ilikuwa damu yake. Kutokana na tatizo hili, Kajanja Komba aliamua kuacha jina lake na badala yake akachukua jina Kajanja Gama ili awe na haki ya watoto aliowazaa na bibi Mzinati. Kimila hawa wanaitwa “Gama wa mali” Mfano wa tatu, mzee Yombayomba Nungu aliishi na Mtepa Gama kwa muda mrefu toka ujana wao. Kila ilipotokea shida walisaidiana kama ndugu kumbe ni marafiki tu. Wakati wa pombe watu walibonga “Yeo Gama” au “Yeo Nungu” Mzee Yombayomba aliona aliona jina Nungu halina heshima kama jina la Gama. Baada ya kufa Mtepa, Yombayomba Nungu aliingia nyumba ya Mtepa kwa makusudi ya kuwatunza watoto wa Mtepa. Hapakuwa na mtu aliyemzuia au kushangaa maana kila mmoja alifahamu uhusiano wa Mtepa na Yombayomba. Ili kuwaonyesha watu kuwa yeye Yombayomba hakuwa rafiki au jirani tu, bali alijifanya kuwa ndugu ya Mtepa, hivyo Yombayomba aliamua kuacha jina la “Nungu” na badala yake akajiita Yombayomba Gama. Kimila hawa wanaitwa “Gama wa Kugula”. Nduna Laurent alionya kuwa hakuna sababu ya kugombana na watu wa aina hiyo.

Iwapo mtu aliamua kujiita GAMA au TAWETE kwa manufaa yake ni bora kumwacha alivyo ingwa kama watu wengine wanajua yeye si Gama au Tawete. Alionya pia kuwa watu wa aina hiyo ni wabaya sana na ni lazima kuangalia katika kushirikiana nao. Mtu kama huyo huhesabiwa kama mgeni asiyeaminika maana anaweza kufanya kitendo kibaya kwa wenyeji ili yeye apate kutawala. Kufuatana na utaratibu wa Wangoni katika utawala wa jadi, Manduna na Majumbe wengi walitoka katika jamaa zenye asili ya Waswazi, Watonga, Wakalanga, Wasenga na Wasukuma. Manyapara walichaguliwa toka makabila mengine yaliyojulikana kwenye vita vya makabila. Hapa chini imeorodhesha ufafanuzi wa Nduna Laurenti kuhusu Wangoni wa Songea kwa ujumla.

Wangoni wenye asili ya WASWAZI: Gama, Tawete, Chongwe, Magagura, Mswani, Maseko, Nyumoyo, Tole, Jere, Mshanga, Masheula, Nkosi, Mlangeni na Malindisa.

Wangoni wenye asili ya WATONGA: Makukura, Silengi, Ntocheni, Sisa, Ntani, Ngairo, Nguo, Matinga, Nkuna, Gomo na Pili.

Wangoni wenye asili ya WAKALANGA: Mbano, Soko, Moyo, Zenda, Newa, Shonga, Shawa, Chiwambo, Hara, Mapara, Mteka na Nyati.

Wangoni wenye asili ya WASENGA: Miti, Mvula, Sakara, Lungu, Tembo, Njovu, Duwe, Nguruwe, Ngómbe, Mwanja na Mumba.

Wangoni wenye asili ya WASUKUMA: Chisi, Ntara, Mpepo, Satu, Zinyangu, Chawa na Mzila.

Wangoni wenye asili ya WANYAME: Nyanguru.
Wangoni wenye asili ya WANDENDEULE: Ngonyani, Mapunda, Ntini, Milinga, Nyoni, Henjewele, Ponera, Luhuwu, Nungu, Mango, Nyimbo, Humbaro, Kigombe, Wonde, Ndomba, Tindwa, Magingo na Luambano.

Wangoni wenye asili ya WAMATENGO: Nchimbi, Ndunguru, Komba, Nyoni, Kapinga, Kifaru, Pilika, Hyera, Mbele, Mkwera, Ndimbo, Mapunda, Ngongi, Mbunda, Kinyero, Nombo na Kumburu.

Wangoni wenye asili ya WAPANGWA: Mhagama, Kihwili, Nditi, Lugongo, Njombi, Mwingira, Kihaule, Mbawala, Njerekela, Komba, Kayombo, Mselewa, Nandumba, Luoga, Luena, Mbena, Mwagu, Mlimira, Sanga, Kokowo, Miloha, Kihuru, Chali, Mwinuka, Nyilili, Mkuwa, Mhonyo, Mkinga, Ngaponda, Goliama na Ng´wenya.

Thursday, May 7, 2009

HATUFANYI KAZI TU KUNA WAKATI HUWA TUNABURUDIKA PIA HAPA NI NGOMA YA LIZOMBE



Napenda kuwakaribisha nanyi pia katika ngoma hii ya asili. Hapa ndugu zanguni ni mpaka lukela mpaka ugimbi umalikayi.

Wednesday, May 6, 2009

TUENDELEE KUANGALIE SURA YA KIJIJI CHA LIKUYU FUSI SEHEMU YATATU = KUNYUMBA

Inaendelea toka sehemu ya kwanza ya Kijiji cha Likuyu Fusi.

Mazao haya yote ni kwa ajili ya chakula chao na kuuza ziada. Baadhi ya wananchi wanalima tumbaku, kwa ajili ya kupata fedha kidogo za matumizi. Wakati wa kiangazi wananchi hulima mboga za aina mbalimbali, kama mchicha, mabogo, nyanya, lipwani, bamia na siku za karibuni wameingiza aina ya mboga za kigeni kama kabeji, saladi, biringanya na aina nyingine. Kwa ujumla kilimo cha mvua za mwaka huwa katika sehemu zalizoinuka na wakati wa kiangazi wananchi hulima mabondeni. Hivyo shughuli za kilimo ni za wakati wote katika mwaka. Mvua za mwaka huanza mwezi Novemba na kumalizika mwezi mei.

Kilimo kimekuwa kwa miaka mingi cha mtu mmoja mmoja au mtu na jamii yake wakishirikiana na jirani wa karibu katika kilimo cha bega kwa bega au “Chama”. Mapato na hali ya maisha ya wakazi kwa ujumla si ya kuridhisha sana. Ingawaje wananchi wanapata chakula kwa wingi cha kuwashibisha lakini kuna uhaba wa vyakula vya aina ya nyama ambayo ni muhimu kujenga miili ya binadamu hasa akina mama wajawazito, watoto na vijana. Vyakula aina ya nyama, samaki, mayai, dagaa, kunde, maharagwe na maziwa ndivyo vinavyojenga miili yetu. Ili watu wajengeke vema kiafya kuna haja ya kuwapa akina mama wajawazito, watoto na vijana vyakula vya aina nilivyotaja kwa wingi.

Kabla ya vita kuu ya pili, wananchi walikuwa na mifugo ya aina mbalimbali, kama ngómbe, mbuzi, kondoo, kuku, njiwa, na bata. Na kwenye mapori kulikuwa na wanyama wa aina mbalimbali kama funo, tambaramba, nguruwe, ngungusi, kwale, kanga, nyani, ngedere, chui na simba na wengineo. Wanyama hawa walikuwa wakiwindwa kwa nyavu, mitego na pengine kwa bunduki za migobole. Hivyo kutokana na mifugo na wanyama wa porini, wananchi waliweza kula nyama mara kwa mara wakati walipotaka. Hivi sasa ufugaji wa wanyama umepungua sana na kadhalika idadi ya wanyama wa porini. Hali hii inaleta shida kubwa ya kupata nyama huko vijijini.

Watu wachache wanofuga wantama hao ni kwa ajili ya posa, misiba, harusi au wakati mwingine kwa ajili ya kuwapata watu kuwalimia mashamba yao ya binafsi. Ufugaji wa kuku na bata nao ni wa kijadi. Kuku huzurura ovyo mashambani wakitafuta panzi, kupelkua mchwa na kutafuta chembe za nafaka mashambani. Hali hiyo hiyo ipo kwenye ufugaji wa bata.

Watu wachache hufuga nguruwe nao pia ni kiasi kidogo sana na matumizi yake makubwa ni kuwalipa watu wanolima wakati wa masika. Kuna uwezekano wa kuongeza ufugaji huu kwani chakula cha nguruwe si vigumu kupatikana.

Kijiji cha Likuyu Fusi kina mafundi wachache wa useremala wenye mashine za kuranda, kupasua mbao, kutengeneza milango, madirisha, meza, viti na madawati nk. Mafundi hawa ambaohupata msaada wa mara kwa mara toka misheni, hufanya kazi zao binafsi ingawaje huwaajiri vijana wa kuwafunza kazi. Siku hizi karibu kila kijiji kilichoandikishwa kimekopeshwa na Benki ya maendeleo vijijini, mashine za kusaga na kukoboa nafaka, matrekta ya kulimia na malori. Hata hivyo ni watu wachache wenye kuzingatia kazi za kilimo, kwani idadi kubwa ya wakazi wa sehemu hizi hutegemea kazi za kuajiriwa na misheni au mahali pengine katika mashirika na Serikali. Katika vijiji nilivyovitaja wapo pia mafundi wa uhunzi wenye kutengeneza mashoka, mikuki, visu, nyengo,vinu n.k. Vitu hivi hutengenezwa kwa kiasi kidogo sana ili kupata fedha za kununua mahitaji na kulipa gharama mbalimbali za maisha. Katika kila kijiji kilichoandikishwa na vile vya asili zimefunguliwa shule moja kutegemea idadi ya watoto walioko. Zaidi ya hayo zipo huduma za madhehebu mbalimbali ya dini katka kila kijiji. Ingawa bado watu wengi hutegemea masoko yaliyoko katika vituo vya misheni, siku hizi kila kijiji kimeanzisha shughuli za soko kama vile uuzaji wa pombe na vyakula, na mazao mbalimbali toka mashambani kwao. Hata hivyo serikali za vijiji zinatakiwa kufanya jitihada kubwa kupunguza tatizo la wizi wa mali za vijiji ambao hutokana na kuwa na majengo hafifu ya kutunzia mali hizo, pamoja na utunzaji mbaya wa mahesabu yake. Wengi wa viongozi wa vijiji hawana ujuzi wa shughuli hizo, na hawapo tayari kutoa nafasi kwa wale wenye uwezo. Hilo ni tatizo la kudumu katika baadhi ya vijiji na limesababisha vijiji hivyo kushindwa kuendelea. Bado ipo haja ya kuwa na msukumo mkubwa sana wa kuwaelimisha wakazi kuhusu uendeshaji wa shughuli za kijiji katika upande wa uchumi.

Jengo la Mahakama lililojengwa wakati wa Nduna Laurent akiwa mtawala wa jadi, bado linaendea kutumika kama mahakama na ofisi ya Mahakama ya Mwanzo.

Wakazi wa vijiji nilivyotaja wanahudumiwa na hospitali kubwa ya Peramiho na Songea. Hata hivyo katika kila kijiji lipo sanduku la huduma ya kwanza ambayo huangaliwa na Serikali ya Kijiji. Zipo barabara kubwa zinazopita katika maeneo ya baadhi ya vijiji lakini hali ya vijiji hivyo bado havijafikia hatua ya kujitegemea katika huduma za usafiri kwa wakazi wake. Malori ya mikopo na matrekta hutumika kwa muda mfupi kutokana na kuharibika mara kwa mara kwa kukosa uangalizi mzuri.

Kama nilivyoeleza hapo juu kuwa eneo la Likuyu Fusi limebahatika kuwa na mito ya kudumu kwa hiyo hakuna tatizo la kukosa maji. Hata hivyo kwa msaada wa Serikali na Misheni baadhi ya vijiji vimepelekewa maji kwa mabomba. Mipango hiyo inaendelea katika vijiji vilivyobaki.

Wakazi wa Likuyu Fusi ni Wangoni wenye asili mbalimbali. Nduna Laurent alikuwa mjuzi wa kupambanua asili zao. Alikuwa anasimulia kuwa siyo kila mtu ni Mngoni wa asili. Watu wengine wanaitwa Wangoni kwa sababu zao mbalimbali. Mathalani, yapo makabila yaliyokuwepo katika nchi hii kabla ya Wangoni wageni hawajaingia Wilaya ya Songea. Makabila hayo ni Wandendeule, Wamatengo,Wamwera,Wahyao, Wamatumbi na Wapangwa, Baadhi ya watu toka katika makabila haya walipewa Ungoni kwa ajili ya kutekwa katika vita vya makabila, na wengine kwa ajili ya kuzaliwa katika mali ya mtu, na wengine walinunua kabila. Mathalani, Mtepa Gama alipokuwa vitani aliteka watumwa wanne, wawili wanawake na wawili wanaume, Hawa wote kila mmoja wao alikuwa na jina lake la ukoo, kama Komba, Hyera, Ngonyani, Kihaule n.k. Watumwa hawa baada ya kutekwa waliruhusiwa kuendelea kutumia majina yao au walitaka waweze kutumia jina la mtu aliyewateka. Ili kulinda usalama wao watumwa hao waliamua kutumia jina la ukoo wa Mtepa ambaye aliwateka na hivyo walijulikana kuwa ni watu wa Mtepa. ITAENDELEA.......

NIMETENGENEZA LORI LANGU NIPO KIJIJI CHA LIKUYU FUSI SEHEMU YA PILI

LIKUYU -PERAMIHO
Mtoto akicheza kuwa anaendesha gari, nadhani wengi itawakumbusha mbali sana hapa ni kijijini Likuyu Fusi

Tuesday, May 5, 2009

NGOJA LEO NIWAPELEKE NA TUANGALIE SURA YA KIJIJI CHA LIKUYU FUSI SEHEMU YA KWANZA= KUNYUMBA

Kijiji cha Likuyu Fusi ni kijiji cha asili cha muda mrefu kilichoanzishwa na kundi la Wangoni wa Luyangweni ya malawi miaka michache baada ya vita vya Majimaji. Kabla ya kuanzisha kijiji hiki wakazi wake waliishi katika eneo la kijiji cha Kilawalawa-Luyangweni ya Mpitimbi, mahali ambapo Bambo Fusi, bin Zulu alihamia na kundi lake toka Malawi.

Kijiji cha Likuyu Fusi kipo upande wa kusini wa kanisa la Misheni Peramiho, umbali wa maili tatu na kipo kusini ya mji wa Songea umbali wa maili kumi na tatu kuelekea barabara iendayo Mbambabay.

Jina la Likuyi Fusi linatokana na mti uitwao “mkuyu” ambao unapendelea kuota katika bonde la mto Likuyu. Tunda la mti huo huitwa “Likuyu” na hupendwa sana kuliwa na baadhi ya ndege. Mto Likuyu unaanzia mlima wa Liwanganjahi na kupeleka maji yake hadi mto Ruwawazi. Urefu wake ni maili nne. Kabla ya kuvuka mto huu katika barabara itokayo Songea kuelekea Mbambabay ulikuwepo mti mkubwa wa mkuyu wenye kivuli kizuri chini yake. Wasafiri wengi walizoea kupumzika na kupika chakula chao chini ya mti huo. Kituo hiki kilikuwa kikubwa na kilijulikana kwa wasafiri wengi waliokitumia. Wasafiri hao walipita mahali hapo “Likuyu” kutokana na matunda ya mti wake. Toka muda huo jina la Likuyu limeendelea kutumika hadi sasa.

Jina la Fusi ni jina la baba mzazi wa Nduna Laurent. Kwa kuwa mto wa Likuyu ulikuwepo katika eneo la utawala wake, wasafiri waliamua kuita mto huo Likuyu Fusi kutofautisha na Likuyu nyingine iliyoko katika sehemu ya Undendeule, katika wilwya ya Songea, ambayo ilitawaliwa na Nduna Sekamaganga.

Kijiji cha Likuyu Fusi kimekuwa ni makao makuu ya utawala wa Nduna Laurent Fusi. Makao haya kwanza yalikuwa kijiji cha Luyangweni ya Mpitimbi na hatimaye yalihamishiwa Likuyu miaka michache baada ya vita vya majimaji.

Utawala wa Nduna Laurent Fusi ulijumlisha wakazi wa vijiji vya asili ya Parangu, Lihongo, Likuyu, Mkurumo, Ruwawazi, Mangúa, Chimbembe, Mlahimonga, Liboma, Mbatamira, Mapera, Litapwasi, Halali Magomera, Halali Fusi, Mhangazi, Matomondo, Kikole na Kilawalawa.

Kijiji cha Likuyu Fusi kina milima miwili na yote ipo upande wa kusini ya kijiji. Mlima Livánganjali upo karibu zaidi na nyuma yake unafuata mlima wa Namakinga. Pia katika eneo la kijiji ipo mito; Lihongo, Likuyu, Litapwasi, Chimbembe, Liboma, Mhangazi, Ruwawazi na Ruvuma. Mito hiyo ina mabonde mazuri kando yake yenye maji ya kutosha kwa wakati wote wa mwaka. Ardhi yake ni kidongo chekundu katika sehemu kubwa na mabonde yake yana udongo wa aina ya mfinyanzi wenye rutuba nzuri. Vilevile vya milima vina mawe mazuri yenye kuzuia mmongónyoko wa ardhi.

Katika maeneo ya vijiji nilivyovitaja ipo miti ya aina mbalimbali, kama miyombo, misuku, miwanga na aina nyingine ya miti midogo midogo. Kwa vile maeneo haya yalikaliwa na watu kwa muda mrefu sehemu nyingi zilizolimwa zamani sasa zimeota manyasi marefu na vichaka vya miti midogo midogo. Mitelemko ya milima na kando kando ya mabonde ya mito bado kuna miti mikubwa kiasi ya aina niliyoitaja hapo juu. Kabla ya matumizi ya mbolea ya chumvichumvi kuenezwa wananchi walikuwa wanafanya kilimo cha kuhamahama wakikata “matema” kila baada ya miaka mitatu au minne. Tabia hii imesababisha kupungua kwa miti katika sehemu zote za tambarare na kuwalazimu wananchi kuanzisha mashamba mapya kwenye mitemko ya milima na hata kwenye vilele vya milima. Mabonde ya mito iliyotajwa hapo juu ina sehemu nzuri ya kilimo cha kiangazi “madimba”. Manyasi, magugu na matete na mimea ya asili ambayo sehemu nyingi hufyekwa wakati wa kiangazi ili kulima mashamba ya madimba.

Wananchi katika sehemu za vijiji nilivyovitaja hulima mahindi, maharagwe,ulezi, mtama, mihogo, viazi vitamu, viazi vikuu mpunga na aina mbali mbali za kunde, kama mbaazi, nandala, fiwi, mangatungu, pia hulima karanga, ufuta, mazomba, aina mbalimbali za matunda kama mapapai, mapera na miembe.Inaendelea........

Monday, May 4, 2009

NAANZA JUMATATU HII NA HUYO DADA NA MITINDO YAKE UKIJIPENDA MWENYWE NA WENGINE WATAKUPENDA=MAISHA

Mimi Nangonyani

Hapa pia mimi nawaza kitu

Hapa nilikumbuka nilipokuwa mdogo nilikuwa napenda sana kufunga nguo (Lubega) shingoni

Sunday, May 3, 2009

UBAGUZI WA RANGI TANZANIA/AFRIKA

Baada ya kusoma mada ya Prof. http://matondo.blogspot.com/aliandika kuhusu Ubaguzi wa rangi Tanzania (inasikitisha sana) nimepata wazo la kuandika kitu hiki
Napatwa na uchungu nionapo/sikiapo sisi waafsika tunavyowaheshimu wenzetu wazungu. Tunavyowanyenyekea na kuwaona ni watu wa maana kuliko sisi wenyewe. Nimewahi kusikia watu wakisema una bahati kuwa pamoja/kuolewa au kuoa mzungu. Yaani wanaona Fahari sana kuwa karibu na mtu mweupe.

Bado sijajua kwanini isiwe bahati kuolewa/kuoa mwafrika kwanini tusijionee fahari rangi yetu. Na kuna wanaofikiri mtu "mweupe" mzungu ni tajiri sana na wana kila kitu. Kwa uzoefu wangu kwa jinsi nilivyoishi hapa nilipo HAPANA. Wao ni watu kama sisi isipokuwa ni rangi tu. Kitu kingine ni kwamba maisha ya hawa wenzetu ni standard nyingine vitu, chakula nk. ni ghali sana. Basi wafikapa Afrika hata kama wana pesa kidogo wanaonekana wana hela nyingi kwasababu vitu na chakula ni bei rahisi kuliko watokako.
Nawaambieni si fahari kuwa /kuolewa au kuoa mzungu. Ukiwa Afrika na hasa mkiwa madukani na sokoni tunauziwa vitu kwa bei kubwa sana kisa nipo na mzungu. Kazi kwelikweli! Hawawezi kufikiri mzungu ni mtu tu wa kawaida.

Siku moja tulikwenda kununua kitanda mimi na mume wangu. Tulipouliza bei wakatuambia ni shilingi laki moja . Siku hiyohiyo baada ya dakika tano hivi tukamtuma kakangu aende kuuliza bei palepale tulipouliza sisi yeye akaambiwa ni shilingi 60,000/=. Kwa kweli ilibidi tucheke, baada ya muda tukaenda na kununua kwa bei hii ya mwisho, alipotuona kuwa ni sisi "wazungu" tena aliona aibu sana .

Nikawa nawaza na kushangaa ni kweli hapa Tanzania yangu au? Kwa kweli inachekesha sana na pia inasikitisha sana kuona Tanzania yetu ipo hivi.

Friday, May 1, 2009

RUHUWIKO 2009 KUTIA MBOLEA KWENYE SHAMBA LA MAHINDI

Niwapo nyumbani huwa nafurahia sana maisha haya ya kujishughulisha na shughuli ambazo nilifanya nilipokuwa mdogo. Nadhani hapo mnaweza kujua huyo mwingine ni nani naye anajitahidi kujifunza mila na desturi.